2012-03-12 15:02:02

Kwaresima kiwe ni kipindi kwa watawa kukuza na kudumisha moyo wa upendo na matendo ya huruma


Kardinali Joào Braz de Avis, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume anawakumbusha watawa kwamba, kipindi cha Kwaresima ni mwaliko kwao wa kukuza na kudumisha moyo wa upendo na matendo ya huruma, hususan kwa watu wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii kutokana na hali yao ya maisha.

Hii ni njia muafaka ambayo Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anawaalika waamini na watu wenye mapenzi mema kuitumia katika kipindi hiki cha Kwaresima kama kielelezo cha toba na wongofu wa ndani. Watawa wanakumbushwa kumwilisha matendo ya huruma katika maisha na utume wao, kama njia ya ushuhuda wa uwepo endelevu wa Mungu kati ya watu wake. Mama Kanisa, anapenda kutoa shukrani na pongezi kwa watawa waliotawanyika sehemu mbali mbali za dunia kutokana na majitoleo yao ya matendo ya huruma kwa maskini na wale wanaoishi vijijini.

Inasikitisha kuona kwamba, idadi ya watawa inazidi kupungua mwaka hadi mwaka, hasa katika nchi za Ulaya, hali ambayo inasababisha pia machungu katika utoaji wa ushuhuda makini. Ufaransa ni kati ya nchi ambazo idadi ya miito na maisha ya kitawa inazidi kupungua kwa kasi ya ajabu. Matatizo, changamoto na fursa zote hizi zitumiwe kikamilifu na Mama Kanisa katika kuchunguza dhamiri ili kuona ni wapi ambapo mambo hayakwenda vyema kadiri ya mpango wa Mungu, ili kujiwekea mikakati ya kuboresha hali kama hii, kwa ajili ya mafao na ustawi wa Mama Kanisa kwa siku za usoni.

Ikumbukwe kwamba, kila mwamini anawajibika kupandikiza mbegu ya miito mbali mbali ndani ya Kanisa kwa njia ya ushuhuda wa maisha adili na matakatifu. Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa namna ya pekee, anawaalika watawa kutolea ushuhuda wa tunu msingi za Kiinjili katika maisha na utume wao; maisha yao hayana budi kwenda sanjari na uhalisia wa maisha wanayoyatangaza mbele ya watu.








All the contents on this site are copyrighted ©.