2011-06-09 08:10:16

Youcat: inavyochambua mafumbo ya imani ya Kanisa Katoliki kwa ajili ya vijana


Ninayo furaha kubwa kukukaribisha tena katika hema letu la vijana leo hii tunapoendelea kuzipembua kurasa za ‘Youcat’, Katekesimu kwa Vijana ambayo Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kapenda kutuandalia. Wiki iliyopita tuliona ni kwa nini binadamu anakuwa na uwezo wa kuamini. RealAudioMP3
Leo hii tutaitazama sehemu ya pili ya mada ya kwanza, ambapo Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anatufundisha juu ya mafumbo makuu ya imani yetu. Ni mafumbo si kwa sababu ni mambo ya maficho tusiyoweza kuyafahamu, bali ni mambo ambayo tunayafahamu ila kwa akili ya kibanadamu hatuwezi kuyafahamu katika ukamilifu wake mpaka pale tutakapokutana na Mungu mwenyewe uso kwa uso ndipo tutaweza kuyafahamu katika ukamilifu wake.
Kanisa limetupatia kanuni ya imani ambamo kuna mafumbo makuu ya imani yetu, baada ya kukili imani tunaitikia AMINA, ishara ya kuyakubali kwa uhuru yale tuliyoyakili. Mafumbo haya tunayokili si maneno au porojo tu za kijiweni, bali ni mambo halisi. Kanisa limeiweka kanuni hii ya imani ili itusaidie kutafakari, kukiri, kujifunza, kurithisha kwa wengine, kuadhimisha na kuyaishi mafumbo haya ya imani yetu.
Kanuni ya imani inatusaidia ili tusiamini wala kutangaza uzushi. Kwa hivi inatusaidia kukiri imani yetu kwa pamoja kama asemavyo mt Ireneo wa Lyon ya kuwa kanisa linailinda imani kama vile linaishi katika nyumba moja, na linaamini kama vile lina roho moja na moyo mmoja, nalo linaitangaza, linaifundisha na kuirithisha kwa wengine kama vile lina kinywa kimoja.
Tunasadiki kwa Mungu mmoja, baba mwenyezi, muumba wa mbingu na nchi na vitu vyote vinavyoonekana na visivyoonekana. Mungu ni mmoja katika nafsi tatu, yaani baba, mwana na roho mtakatifu. Mungu si mpweke, bali anaishi kwenye umoja mkamilifu wa upendo katika utatu mtakatifu, kwani Mungu ni Upendo (IYohane 4,8; 16). Mt. Augustino anatufundisha kuwa palipo na upendo lazima pawe na utatu, yaani mwenye kupenda, mwenye kupendwa na chanzo chenyewe cha upendo.
Tunamwita Mungu baba mwenyezi sababu ndiye muumba wa vyote na anatujali wote kwa upendo wa kibaba, hata Kristo mwenyewe katufundisha kumwita baba (Mathayo 6,9) na kama anavyotufundisha mtakatifu Paulo ya kuwa sisi tumeipokea roho ya kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia Aba, yaani baba (Warumi 8,15). Mungu ni muumba kwa sababu vitu vyote vimetokana na utendaji wake.
Kuhusu nadharia juu ya ubadilikaji au ukuaji wa kimaumbile, kwa mtazamo wetu wa kikristo ni kwamba hata katika mabadiliko hayo ni kazi ya Mungu mwenyewe ambayo inaendelea kupitia maumbile. Mungu kaumba vitu tunavyoviona mfano mbingu, ardhi, maji n.k; na kaumba pia vitu tusivyoviona mfano pumzi au roho.
Tunaamini kwa Yesu Kristo, Mungu kweli na mtu kweli, mkombozi wa ulimwengu. Aliyetungwa mimba kwa uwezo wa roho mtakatifu na akazaliwa na bikira Maria. Na ili kutuokoa kutoka katika utumwa wa dhambi baada ya kuanguka kwa wazazi wetu wa kwanza, ilimlazimu kusulubiwa msalabani. Siku ya tatu, Mungu akamfufua kutoka wafu kama mzao wa kwanza wa waliolala mauti. Kristo katuonesha upendo mkuu na wa ajabu, yaani nia ya Mungu kuishi na mwanadamu na utayari wake kusulubiwa na kukionja kifo ili kutukomboa. Kristo katufundisha ni jinsi gani tunapaswa kuishi kama wanadamu ili tuweze kuishiriki mbingu.
Amepaa kwenda mbinguni na ameketi kuume kwa Baba naye atarudi tena kwa hukumu ya mwisho. Mbingu si mahali bali ni hali ile ya kuwa katika umoja na upendo na mwenyezi Mungu. Kila mmoja napofariki roho yake hupata hukumu binafsi, na katika ile hukumu ya mwisho atakapokuja tena Kristo, kutakuwa na hukumu ya jumla kwa ulimwengu mzima. Tunaamini kuwa Bikira Maria ni Mama wa Mungu, maana ni kwa uwezo wa Roho Mtakatifu kampokea yesu katika tumbo lake la uzazi, Kristo aliye Mwana wa Mungu.
Yeye hakuwahi kumjua mwanaume. Sababu kwa pamoja na mchumba wake Yosefu, Baba mlishi wa Yesu Kristo, walipenda kuishi hivyo maisha yao yote. Bikira Maria kwa neema ya pekee na kwa mapenzi ya mwenyezi Mungu na kwa mastahili ya Kristo mwanae mkombozi wa ulimwengu alikingiwa dhambi ya asili ili asiwe na doa la dhambi.
Mpenzi msikilizaji, ni kama vile unapofikia katika utamu wenyewe wa utafunaji mua, inakuwa ngumu kuuachia. Ndivyo tulivyo kwa sasa tupo katika uhondo wenyewe wa kuyachambua mafumbo ya imani yetu kama anavyotufundisha baba mtakatifu. Lakini kama unavyojua mambo mazuri hayahitaji haraka, na ukitaka kujipa raha jitulize.
Ni taaaaratibu nikiondoka kwa mwendo wa kinyoga mpaka hapo wiki ijayo katika mida na nyakati kama hizi, si mwingine bali mhudumu wa Altare ya Bwana Celestin Nyanda.








All the contents on this site are copyrighted ©.