Ijumaa Kuu: "Mnyonge mnyongeni, lakini haki yake mpeni"
Mama Kanisa siku ya Ijumaa kuu anatafakari kwa kina mateso ya Yesu Kristo Msalabani,
changamoto kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kusimama kidete kulinda na
kutetea: utu, heshima na haki msingi za binadamu. Mheshimiwa Padre Alcuin Nyirenda
anahitimisha tafakari ya kina katika Juma hili takatifu kwa kibwagizo kifuatacho "mnyonge
mnyongeni, lakini haki yake mpeni".
Ndugu zangu,
Siku kuu ya Pasaka ni kubwa sana, kudhihirisha uzito huo, tumepewa kipindi kizima
cha siku arobaini, (kwaresima) kujiandaa ili tuweze kujipatanisha na Mungu. Katika
kipindi hicho cha kwaresima tumevisikia vituko mbalimbali vilivyopelekesha Yesu kusakwa
hadi kushikwa, halafu kumtesa, na kumhukumu, na kumnyonga msalabani hadi kufa.
Katika
juma hili kuu, tumeona mambo mbalimbali yanayokera na kukirihisha sana moyo aliyotendewa
Yesu na waumini wa dini wakiwa makuhani na wafuasi wake. Unaweza kubunia ni kosa gani
la jinai alilolifanya Yesu hadi akastahili adhabu kifo? Alitenda kosa gani lililowakasirisha
watu wengi hivi hata ikabidi kufanyike hata msako wa kumwua bila kuthamini uhai wake?
Hivi Yesu alifanya tendo gani bovu hadi rafiki zake wakamsaliti?
Alifanya
tendo gani la jinai hadi watu waliobobea kwa imani ya dini yao waweze kuvunja amri
ya Mungu wao ya kutesa na kuua? Hakuna ambaye angeweza kufikiria kwamba maisha ya
Yesu hapa duniani yangetamatika hivyo. Vitendo alivyotendewa Yesu na maneno ya karaha
aliyonenewa Yesu ambayo yanakera katika Injili ya leo ni kwanza Yesu kuzabwa kofi,
halafu na lugha aliyopewa na mtumishi wa kuhani. Ninashindwa kupata picha, namna gani
binadamu anathubutu kumzaba kofi Mungu, mwumbaji wake, Bwana Yesu Kristu, aliyekuwa
daima mwenye upendo na huruma kwa watu wote hapa duniani.
Hebu leo tulione
suala hili la Yesu kupigwa kofi. mazingira yepi yaliyompelekesha Yesu hadi akazabwa
kofi? Yesu baada ya kukamatwa alipelekwa moja kwa moja kwa kuhani Anasi ambaye Yohane
anasema alikuwa ni mkwe wa kuhani mkuu Kayafa. Yaonekana makuhani hawa walikuwa pia
na madaraka fulani ya kiserikali kadiri ya sheria ya warumi, ndiyo maana walipelekewa
mhalifu kama Yesu ili wamhoji. Waliofaulu kuingia ndani alikokuwa kuhani ni Yohani
kwa sababu alijulikana na kuhani (labda walikuwa ndugu), wengine kama Petro walibaki
nje wanaota moto.
Kuhani alipomwuliza Yesu juu ya sera zake na juu ya wafuasi
wake. Jibu la Yesu lilikuwa dhahiri kabisa kwamba yeye sera na mafundisho yake makuu
ya ufunuo yalikuwa ya hadhara. Sera zake alikuwa anazimwaga pale anapoona imekusanyika
lukuki ya watu, hivi hakuna mficho wala ubaguzi, ndivyo alivyoweza kupeleka ujumbe
wake wa ukweli na haki kwa watu wote bila kuogopa dola wala dini ya mtu. “Mimi nimesema
na ulimwengu waziwazi…wala sikusema neno lolote kwa siri. Ya nini kuniuliza mimi?
Waulize wale waliosikia niliyowaambia; wao wanajua niliyoyanena.” (Yoh. 18:21).
Maneno
haya ndiyo yaliyomchefua nyongo mtumishi mmoja ambaye kutokana na ushabiki na unafiki
kwa Kuhani, akamzaba Yesu kofi, na kumwonya “Ndiyo majibu hayo kwa kuhani mkuu?” Hapa
Yesu anashindwa kunyamaa kudhalilishwa na kunyongewa hivi haki yake ya kusema ukweli
na haki anaona bora akanyweshe katumishi haka vidonge vyake. Jibu la Yesu la heshima
ni fundisho kuu na laweza kuwa maelezo kwa msemo huu: “Mnyonge umnyongee lakini haki
yake mpe. “Kama nimesema vibaya, ushuhudie ule ubaya; bali kama nimesema vema, wanipigia
nini?” Hapa Yesu hakatai kupigwa kofi, maana alisema “mmoja akikupiga kofi la mkono
wa kushoto mgeuzie na la kuume” (Mt. 5:39; Lk. 629).
Hapa lakini, Yesu anataka
kuonyesha kwamba kipigo alichopata ni uhalifu, uhasama, uonezi, ametendewa jeuri kutokana
na unyonge wa kutoweza kujitetea kwa vile amefungwa. Lakini ukweli hana kosa lolote.
Hivi ndivyo wanavyotendewa wanyonge wasioweza kujitetea. Yesu anataka kuonyesha kwamba
mnyonge yabidi atambuliwe daima na popote. Tendo lolote la ubabe dhidi ya mnyonge
ni matumizi mabovu ya madaraka na mamlaka. Hivi anamwalika kijana kutumia akili yake
na kutoa hoja kabla ya kuwaonea wanyonge: “Kama nimesema vibaya, ushuhudie ule ubaya”.
Tamko hili la Yesu kwa undani wake ni kama “kugeuza shavu la pili”, yaani, amesamehe
lakini kusamehe huko hakufuti tendo aliloishatendewa. Halafu Yesu anaendelea kuuliza
swali, “kama nimesema vema, wanipigia nini? Maneno haya yanawaendea wengi, yanamwendea
Askari aliyemtenda vibaya, wale waliomhukumu kufa. Sanasana ni mwaliko kwenye tafakari
juu ya kukoseana haki na juu ya udhulumu usioweza kuelezeka dhidi ya wanyonge.
Imepita
tayari miaka elfu mbili na ushehe toka Yesu alipouliza swali hili: “Kwa nini wanipiga?”
Swali hili linatoa nguvu kwa watu wote kutetea haki na ukweli vinapovunjwa, iwe katika
familia katika serikali, katika dini, hasahasa dhidi ya wanyonge. Msimamo wa Yesu
dhidi ya wanyonge na umuhimu wa kuizungumzia misingi ya haki za binadamu ndiyo jibu
lililo kwenye roho ya ndani kabisa ya kusamehe ya upendo ambayo tunaikuta katika Injili
ya leo.
Kwa vyovyote hata ukijua kusamehe na kupenda huko hakumaanishi kuukana
uonevu na kukoseana haki ambako kunasababisha uovu. Msimamo huo wa Yesu una maana
sana katika maisha yetu: yaani kuwatetea maskini, wadhaifu, wanyonge, wale wote wanaolowa
damu kutokana na kudhulumiwa na viongozi na mataifa makubwa. Haitoshi tu kuwatetea
wanyonge, bali yabidi pia kutetea haki, yaani haki ya kila mmoja na siyo kusubiri
hadi yatokee madhulumu na uonezi wa hao wakuu ufanyike ndipo tuanze kutangaza uhuru
na kuheshimiana na kujaliana.
Mateso ya Yesu ni hasa kule kugandamizwa na
maamuzi ya kikandamizaji yasiyojali utu wa mtu, hata kama mtu huyo ni mnyonge na asiye
na hatia yoyote kabisa, lakini ananyongewa na kuuawa. Swali la Yesu linagusa moja
kwa moja dhamira ya kila mtu mwenye mapenzi mema (wa kila dini ya kweli), la kutetea
heshima na haki ya wanyonge.
Leo Yesu anatuuliza sisi swali hilo. “Kwa nini
wanipiga?” Endapo hatumpigi mwilini, je tunajeruhi Moyo wake Mtakatifu kutokana na
kushindwa kukabiliana na uovu wa ulimwengu? Je, hatumpigi Yesu usoni pale tunaposhindwa
kuwaonyesha upendo wengine? Je, hatumnyimi chakula Yesu pale tunaposhindwa kuwapa
chakula wenye njaa. Je, hatumfukuzi Yesu, pale tunaposhindwa kuwakaribisha wageni?
Tunaposhindwa kuwahudumia wagonjwa na kwenda kuwaona wafungwa?
Ndugu zangu,
Yesu alisema: “Kweli nawaambieni, yeyote mliyomtendea mmoja wa ndugu zangu, mmenitendea
mimi.”[Mt. 25:40] Je, wiki iliyopita, au mwezi na mwaka uliopita ulimpiga Yesu? Tusiwaonee
wanyongee kwani tunajitia wenyewe upumbavu na kushindwa kujibu swali la Yesu “wanipigia
nini?”. ndivyo, basi tujionee huruma wenyewe! Yesu ni mwenye huruma daima, tumebahatika
naye kupewa Sakramenti ya Kitubio tunamoweza kwenda kusafisha mioyo yetu iliyochafuka
kutokana na uovu tulioutenda dhidi yake.
Leo na kesho, Kanisa linatupendekezea
kufunga kwa ajili ya kushiriki mateso na kifo cha Bwana Yesu, ili kujiandaa wenyewe
vizuri kushiriki kikamilifu na kwa dhati furaha na utukufu wa Ufufuko.