2010-12-30 08:45:34

Askofu Shao wa Jimbo Katoliki Zanzibar asema: utamadunisho ni changamoto inayolikabilia Kanisa Barani Afrika


Mababa wa Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu, katika mapendekezo yao kwa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita anayoendelea kuyafanyia kazi, ili hapo mwakani, Mwezi Novemba, aweze kutangaza matunda ya Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu wa Afrika, walilaani na kukemea vikali mila na desturi mbaya Barani Afrika ambazo zimepelekea kuvunjika kwa misingi bora ya utu na maadili mema. Wanaendelea kukazia majadiliano ya kidini na kiekumene kama njia ya kujenga haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati ndani ya jamii. Wanalaani na kukemea misimamo mikali ya kiimani, ambayo imepelekea mara nyingi kuvunjika kwa amani na upendo kati ya watu.

Mababa wa Sinodi wanaendelea kuhimiza umuhimu wa Uinjilishaji kwa njia ya ushuhuda wa maisha na tunu msingi za kikristo kwa kukazia: uwazi, ukweli na kuheshimiana pamoja, sanjari na mchakato wa majadiliano ya dhati yanayozingatia kweli za Kiinjili. Kanisa Barani Afrika linajitambua kuwa ni Familia ya Mungu inayowajibika, changamoto kubwa ni kuhakikisha kwamba, linaendelea kuwa ni kielelezo amini cha upatanisho, haki na amani; kuwa kweli ni chumvi ya dunia na mwanga wa mataifa.

Askofu Augustine Ndeliakyama Shao wa Jimbo Katoliki Zanzibar katika mahojiano na Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican anasema utamadunisho ndani ya Kanisa Barani Afrika ni dhana au mchakato unaoweza kuwasaidia waamini kuweka misimamo ya maisha ya kidini na kiimani katika uhalisia wake; kwa kuchukua tunu njema, mila, desturi na tamaduni nzuri toka katika maisha ya kiafrika na kuzimwilisha kadiri ya kweli za Kiinjili.

Anasema, mila, desturi na mapokeo potofu yaliyopitwa na wakati, zinapaswa kuachwa, ili kukumbatia mwelekeo mpya wa Kiinjili, ili kuondokana na dhana ya uwili katika maisha ya kikristo; ili hatimaye, kuwawezesha wakristo kutolea ushuhuda imani yao katika medani mbali mbali za maisha.

Ili kufanikisha azma hii, kuna haja ya kujenga misingi ya majadiliano ya kweli katika: dini kwa kujifunza undani wa dini asilia kwani hii ni sehemu ya maisha ya watu wenyewe, bila kusahau kuangalia mila na desturi za watu na maisha yao kwa ujumla. Lengo ni kukoleza dhana ya utamadunisho ndani ya Kanisa. Ninakualika sasa kwa heshima na taadhima kubwa, ukae kitako ili uweze kumsikiliza kwa makini Askofu Augustino Ndeliakyama Shao wa Jimbo Katoliki Zanzibar katika akifafanua zaidi. RealAudioMP3







All the contents on this site are copyrighted ©.