2010-11-16 10:00:19

Mheshimiwa Sana Padre Sosthene Ayikuli Udjuwa ateuliwa kuwa Askofu wa Mahagi-Nioka, DRC


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, amemteua Mheshimiwa Sana Padre Sosthene Ayikuli Udjuwa, msimamizi wa kitume Jimbo Katoliki la Mahagi- Nioka kuwa Askofu mpya wa Jimbo la Mahagi-Nioka, Jamhuri ya Kidemokrasia ya watu wa Congo.

Askofu mteule Ayikuli Udjuwa, alizaliwa tarehe 7 Julai, 1963 huko Faradje. Baada ya masomo yake ya shule za Sekondari, kati ya mwaka 1985 hadi 1988, aliendelea na majiundo ya falsafa huko Kisangani na masomo ya kitaalimungu, aliyapatia huko Bunia, kati ya Mwaka 1988 hadi 1993. Tarehe 15 Julai, 1993 akapewa daraja takatifu ya Upadre.

Tangu wakati huo, alibahatika kufanya kazi mbali mbali ikiwa ni pamoja na kufundisha Seminari Ndogo ya Yohane wa Ishirini na tatu huko Mahagi-Nioka. Baadaye alijiendeleza kwa masomo ya juu katika Sheria za Kanisa, Kwenye Chuo Kikuu cha Kikatoliki, Kinshasa. Akawa ni jaalimu wa Taalimungu kwenye Taasisi ya Mtakatifu Cyprian huko Bunia.

Baada ya masomo yake ya uzamivu wa sheria za Kanisa, toka Chuo Kikuu cha Kipapa cha Laterani, kilichopo mjini Roma, kunako mwaka 2009 alirudi nyumbani na kuteuliwa kuwa ni Msimamizi wa Jimbo Katoliki la Mahagi-Nioka, DRC.







All the contents on this site are copyrighted ©.