2010-10-18 08:42:00

Watakatifu wapya wanalipamba Kanisa kwa mifano ya maisha yao na udumifu katika sala


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Jumapili tarehe 17 Oktoba, 2010, kwenye Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, uliofurika kwa waamini na mahujaji kutoka pande mbali mbali za dunia, aliwatangaza wenyeheri sita kuwa watakatifu. Watakatifu wapya wanaolipamba Kanisa kwa mifano ya maisha na udumifu wao katika sala ni: Stanislaw Soltys Kazimierczyk, Andrè Bessette, Candida Maria De Jesùs Cipitria y Barriola, Mary MacKillop, Julia Salzano na Battista Varano.

Katika mahubiri yake, Baba Mtakatifu amekazia umuhimu wa kusali na kudumu katika sala, kama sehemu ya mafundisho msingi ya Jumapili ya ishirini na tisa ya kipindi cha Mwaka wa Kanisa, kwa kutambua na kuendelea kuthamini umuhimu wa sala katika maisha na utume wa Kanisa.

Baba Mtakatifu anasema, kwa bahati mbaya watu wanadhani kwamba, kwa nguvu zao za kibinadamu bila msaada kutoka kwa Mwenyezi Mungu wanaweza kufanikisha malengo yao. Ni changamoto kwa waamini pia kuhakikisha kwamba wanakuwa ni watu wa haki kwa kutenda haki, hasa kwa wanyonge na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii kutokana na hali yao ya maisha.

Baba Mtakatifu anawakumbhusha waamini kuwa: Mwenyezi Mungu ni kielelezo cha ukarimu na huruma na daima yuko tayari kusikiliza kwa makini kilio cha waja wake katika sala, changamoto kwa waamini kutokata tamaa katika sala, bali kujenga utamaduni wa kudumu katika kusali, kama Kristo mwenyewe anavyohimiza. Sala katika undani wake ni kielelezo cha imani katika wema wa Mungu anayemlipa kila mmoja kadiri anavyopenda. Huu ni msingi wa maisha ya sala, kama inavyojionesha katika maisha ya watakatifu waliotangazwa siku ya Jumapili kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican.

Mtakatifu Stansilaus, mtawa aliyeishi kunako karne ya kumi na tani ni mfano wa mtu aliyeyamimina maisha yake katika Ibada kwa Ekaristi Takatifu. Ni mtu aliyejifunza kutoka kwa wazazi imani na maisha ya ibada; akawa mtawa; akatekeleza wajibu wake kama Padre na mwalimu, akiwa makini zaidi kwa mahitaji ya watu maskini zaidi. Alionesha upendo wa pekee kwa Kristo wa Ekaristi Takatifu, akamwona Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka, anayeendelea kujitoa katika Sadaka ya Misa Takatifu, kama kielelezo na msukumo wa pekee kwa upendo wa Mungu na jirani, chemchemi ya umoja.

Bruda Andrè Bessette alizaliwa nchini Canada, mtawa wa Shirika la Msalaba Mtakatifu, ni mtu aliyeonja makali ya umaskini katika utoto wake, akajifunza kumgeukia Mungu kwa maisha ya ndani zaidi, akawaonjesha saburi wote waliotumaini maombezi yake. Kwa uelewa wake, alijitahidi kuyafahamu yale yaliyokuwa msingi kwa ajili ya imani yake, akajifunza kujiachilia kutimiza mapenzi ya Mungu katika maisha yake. Alijitahidi kumwilisha heri za Kiinjili katika maisha yake kwa njia ya unyenyekevu kwa Mungu.

Ni mtu aliyefanikisha ujenzi wa Madhabau ya Mtakatifu Yosefu, akawa mlinzi wake hadi mauti ilipomfika kunako mwaka 1937. Mahali hapa akawa ni shahidi wa nguvu ya uponyaji na wongofu wa ndani, daima aliwahimiza wakristo kuwa na subira katika majaribu ya maisha yao na kamwe wasiombe kuondolewa bali waombe neema na baraka ya kuweza kuyabeba kwa imani na matumaini makubwa. Ni mkristo aliyejitahidi kumfatuta Mungu katika unyenyekevu wa maisha yake ya kila siku, changamoto kwa waamini kutoka Canada.

Mtakatifu Candida Maria, alikirimiwa kuwa na fadhila ya unyenyekevu tangu mwanzo wa maisha yake, akabahatika kuwapata mapadre waongozi wa kiroho kutoka Shirika la Wayesuiti, kiasi cha kumfanya kutoa kipaumbele kwa Mwenyezi Mungu, akaendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu hata alipoitupa mkono dunia. Aliyatoa maisha yake kwa Mungu na akawaonjesha upendo wake wa dhati maskini na wote waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa jamii wakati huo. Akajitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya majiundo ya wasichana na wanawake wa nyakati zake, kiasi cha kuwa ni mwanzilishi wa Shirika lake, changamoto ya maisha kwa waamini wengine ndani ya Kanisa.

Mtakatifu Maria MacKillop, enzi ya uhai wake, aliwahimiza waamini kuwatambua na kuwathamini waalimu wao wa imani, waliowashirikisha hekima inayowakirimia wokovu na maisha ya uzima wa milele. Baba Mtakatifu anasema, vijana wengi nchini Australia wamebahatika kufundishwa na walimu wanaojitahidi kuiga mfano na ujasiri wa Mtakatifu huyu, kwani hao ndio watawa waliojiunga naye katika harakati za kutoa elimu kwa watu maskini nchini Australia.

Ni mwanamke aliyejitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya vijana waliokuwa wamedhaminishwa kwake, bila kujali matabaka au utajiri wao, wote wakabahatika kupata majiundo ya kiroho na kiakili.

Licha ya changamoto mbali mbali alizokumbana nazo katika maisha yake, lakini, daima kwa njia sala alikimbilia maombezi ya Mtakatifu Yosefu na akajifunza kujificha kwenye Ibada ya Moyo Mtakatifu wa Yesu, kiasi cha kuliweka Shirika lake, chini ya ulinzi na usimamizi wa Moyo Mtakatifu wa Yesu, akabahatika kubaki mwaminifu kwa Kristo na Kanisa lake, changamoto kwa waamini kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya hudjma kwa Mungu na Kanisa kwa njia ya imani na unyenyekevu.

Julia Salzano ni mwalimu wa shule ya msingi, aliyeishi kunako karne ya kumi na tisa, huko Kusini mwa Italia, aliyeitwa kwa neema za Mungu kuwa ni mtume hodari wa Kanisa katika sekta ya elimu, akabahatika pia kuwa ni mwanzilishi wa Shirika la Watawa Makatekista wa Moyo Mtakatifu wa Yesu. Ni mtu aliyetambua na kuthamini katekesi katika maisha na utume wa Kanisa, akajitahidi kuunganisha mbinu za kufundishia, jambo lililomwezesha kuwa na ari katika utume wake, akajitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya majiundo ya watu wa kila umri na tabaka.

Ni mtawa aliyetamani kufundisha katekesi hadi dakika yake ya mwisho ya maisha yake hapa duniani, kwa kutambua kwamba, Mungu alimuumba mwanadamu ili amtambua, ampende na kumhudumia katika maisha yake, kama mambo yanayopaswa kupewa kipaumbele katika maisha ya mwamini. Baba Mtakatifu anasema, mfano wa Mtakatifu Julia Salzano ni changamoto kwa Mama Kanisa kuendelea kumtangaza Kristo sanjari na kuunda dhamiri nyofu za waamini.

Mtakatifu Battista Camila Varano, ni mtawa wa Shirika la Waklara aliyeishi kunako karne ya kumi na tano, kielelezo makini cha ushuhuda wa maana ya maisha ya Kiinjili na udumifu katika sala. Akiwa na umri wa miaka ishirini na tatu, akawa ni kati ya wakereketwa wa maisha na karama ya Mtakatifu Clara wa Assis, akawa ni muasisi wa nyumba nyingine za kitawa na mkuu wa nyumba kwa nyakati mbali mbali. Akajitoa biula ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu, watawa na jirani zake katika fadhila ya upendo, akijichotea baraka na nguvu katoka katika Moyo Mtakatifu wa Yesu. Ni mtawa aliyeyachimbia maisha yake katika toba na sala, akijitahidi daima kuleta mabadiliko ndani ya Kanisa.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, alihitimisha mahubiri yake, kwa kuwaalika waamini kumtolea Mwenyezi Mungu utenzi wa shukrani kwa utakatifu wa maisha, unaoendelea kung'aa ndani ya Kanisa kwa njia ya ushuhuda wa watakatifu wapaya waliotangazwa na Mama Kanisa siku ya jumapili. Ni changamoto kwa waamini kuendelea kuongozwa na mfano wa maisha yao ili maisha ya kila mwamini uwe ni utenzi wa sifa kwa Mwenyezi Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.