2009-10-16 09:20:20

Waathirika wa Ukimwi Uganda ni kielelezo cha upendo wa mshikamano, watu wapya katika imani!


Askofu Beatus Kinyaiya wa Jimbo la Mbulu, Tanzania anasema, uharibifu wa mazingira unatishia mistu na uoto wa asili Barani Afrika na matokeo yake yake ni madhara yanayoendelea kujitokeza sehemu mbali mbali ya Bara la Afrika. Ukame wa kutisha, mafuriko, mmomonyoko wa udongo na athari zake kiasi cha kuwafanya watu kuwa ni wahanga wa mabadiliko ya tabianchi. Binadamu ajifunze kulinda na kutunza mazingira kwa ajili ya kizazi hiki na kile kijacho.

Watalii kutoka sehemu mbali mbali za dunia wamechangia katika shughuli za kiuchumi Barani Afrika, lakini jambo la kusikitisha ni kwamba, Kanisa Barani Afrika alikutumia fursa hii kama sehemu ya Uinjilishaji kwa kuhakikisha kwamba, watalii wanasaidia katika mahitaji yao ya maisha ya kiroho.

Ni jukumu la Mababa wa Sinodi kuangalia uwezekano wa kuteuwa mapadre watakaowasaidia watalii katika mahitaji yao ya maisha ya kiroho wanapotembelea Bara la Afrika.

Sr. Mary Anne Felicitas Katiti, Mama mkuu wa Kanda wa Shirika la Dada Wadogo wa Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili, amewasihi Mababa wa Sinodi kuendelea kuwathamini wanawake katika huduma kwa Kanisa na jamii wanaposhiriki katika azma ya Uinjilishaji wa kina.

Ni watu wanaoteseka na kubeba magumu ya maisha ya kifamilia na kwa kiais kikubwa wao wamekuwa ni wahanga wa nyanyaso za kijinsia. Wanawataka wanaume kuondokana na mfumo dume unaowakandamiza na kuwanyima haki zao msingi.

Yesu Kristo alileta mapinduzi ya kweli katika kumkomboa mwanamke, kiasi cha kuwashirikisha katika utume wake, wanawake wakawa wa kwanza kupokea Habari Njema ya ufufuko wa Kristo. Wanawake wanasubiri haki na heshima kutoka ndani ya Kanisa na Jamii kwa ujumla.

Mama Rose Busingye, m wanzilishi na Rais wa Meeting Point International, kutoka Kampala, Uganda anasema imani haina budi kupenya katika maisha ya mwanadamu, ili iweze kumwilishwa na kutolewa ushuhuda wa maisha kwa ajili ya mafao ya wengi pamoja na kukoleza furaha, haki na amani.

Ili kufanikisha mchakato wa ujenzi wa upatanisho, haki na amani, mwanadamu na mahitaji yake msingi hana budi kupewa kipaumbele, kwa kuthamini zawadi ya maisha na kuenzi utu na heshima ya mwanadamu. Huu ndio msaada mkubwa unaoweza kutolewa na Mama Kanisa Barani Afrika.

Imani anasema Mama Rose Busingye ambaye amekuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi kwa kuonesha mshikamano na waathirika inaweza kumletea mtu mabadiliko. Huu ndio muujiza wa imani kwa waathirika wa Ukimwi nchini Uganda ambao wanaendelea kufanya kazi kwa ajili ya kujipatia riziki yao ya kila siku, licha ya magumu wanayokabiliana nayo.

Ni watu wanaoendelea kuonesha moyo wa mshikamano na watu wengine wanaoathirika kwa majanga asilia sehemu mbali mbali za dunia. Wanatambua kwamba, moyo wa mwanadamu ni wa kimataifa hauna rangi wala kabila.







All the contents on this site are copyrighted ©.