Ndoto ya kufikia Malengo ya Mendeleo ya Millenia yazidi kuyoyoma
Hati ya tatu ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita Caritas In
Veritate, Upendo katika Ukweli, inachambua kwa kina masuala mbali mbali ya kijamii
mintarafu Mwanga wa Injili na ukweli katika kufanikisha Malengo ya Maendeleo ya Millenia,
ifikapo mwaka 2015, jambo ambalo kadiri ya wachunguzi wa masuala ya kijamii, ni ndoto
kuweza kufikiwa kutokana na mwenendo wa hali ya uchumi wa kimataifa kwa sasa.
Social
Watch, Shirika la Lisilo la Kiserikali linalojihusisha na masuala ya kijamii linatabiri
kwamba, pengine Malengoo ya Maendeleo ya Millenia kwa Afrika yanaweza kufikiwa, hapo
mwaka elfu mbili na ishirini, na Asia ya Kati inaweza kufikia Malengo hayo ifikapo
mwaka elfu mbili na arobaini. Wimbi la umaskini linazidi kuongezeka maradufu duniani,
tofauti kabisa na takwimu zilizokuwa zimetolewa na Benki ya Dunia kwa mwaka elfu mbili
na nane.
Hali ya maisha kijamii kwa watu wanaoishi Kusini mwa Jangwa la Sahara
inazidi kudorola ikilinganishwa na miaka kadhaa iliyopita. Haya ni matokeo ya mfumuko
wa bei ya mazao ya chakula iliyojitokeza mwaka 2006, kupanda kwa gharama ya nishati
pamoja na kuchechemea kwa uchumi wa kimataifa. Yote haya yanapelekea kutofikiwa kwa
Malengo ya Maendeleo ya Millenia, kama ilivyokuwa imepangwa na Umoja wa Mataifa kwa
Mwaka 2015.
Social Watch, inazitaka nchi tajiri kufanya mabadiliko makubwa
katika kukabiliana na mtikisiko wa kiuchumi, kusaidia kuboresha hali ya usalama wa
chakula kwa nchi changa, matumizi ya nishati salama na rafiki kwa mazingira na udhibiti
wa uchafuzi wa mazingira duniani. Yote haya yajengeke katika msingi wa haki na ushirikiano
wa kimataifa, kwa lengo la kuboresha hali ya uchumi wa kimataifa na madhara yake kwa
nchi zinazoendelea duniani.
Umoja wa Mataifa ulikuwa umejiwekea Malengo ya
Maendeleo ya Millenia ifikapo Mwaka 2015, ili kutokomeza balaa la njaa, umaskini,
utoaji wa elimu kwa wote, kupunguza vifo vya akina mama wajawazito na watoto wenye
umri mdogo, kukuza usawa wa kijinsia, kuboresha mazingira, kupambana na ukimwi pamoja
na malaria, magonjwa ambayo yamekuwa ni sababu ya vifo vya watu wengi katika Nchi
Zinazoendelea.
Uchafuzi wa mazingira, ukame wa kutisha, ongezeko la Jangwa
Kusini mwa Sahara na kwamba, kuna watu zaidi ya millioni mia moja na thelathini na
tano, katika kipindi cha miaka kumi kuanzia sasa hawatakuwa na makazi. Watu zaidi
ya Billioni moja nukta mbili hawapati huduma ya maji safi na salama. Na kwamba, kuna
watu Billioni mbili nukta nne, hawapati huduma ya afya ya msingi duniani.
Nchi
wahisani wamepunguza kwa kiasi kikubwa mchango wao kwa ajili ya kugharimia Malengo
ya Maendeleo ya Millennia. Wachunguzi wa masuala ya kiuchumi wanasema, kuna haja pia
kwa wahisani kuratibu na kuhakikisha kwamba, misaada inayotolewa kwa nchi zinazoendelea
inawafikia walengwa, vinginevyo, inaweza kuishia kwenye mikono ya mafisadi na wahujumu
uchumi.
Hati ya tatu ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na
sita inayaangalia masuala ya kijamii na kujitahidi kutoa mwelekeo wa matumaini, ili
dunia iendelee kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.