2009-03-25 09:40:43

Utamaduni wa upendo na mshikamano kuwafaidisha Watoto wa Kijiji cha Matumaini Dodoma na Hospitali ya Mt. Gaspar, Itigi


zaidi ya Euro hamsini na tatu elfu zimekusanywa na wanachama wa Chama cha Ushirika cha Legnaria, kilichoko mjini Firenze, Kaskazini mwa Italia, ili kuonesha mshikamano wa upendo na wananchi wa Tanzania katika utoaji wa huduma kwa wagonjwa na watoto walioathirika kwa virusi vya Ukimwi.

Kitivo cha Kilimo cha Chuo Kikuu cha Firenze kwa kushirikiana na wadau mbali mbali wamekusanya fedha zitakazotumika kuendeshea shughuli za huduma ya elimu, tiba, chakula na malazi kwa watoto zaidi ya mia moja hamsini wanaoishi na virusi vya ukimwi na kuhudumiwa kwenye Kijiji cha Matumaini, kinachomilikiwa na kuendeshwa na Masisita Waabuduo Damu Takatifu ya Yesu.

Hospitali ya Mtakatifu Gaspar iliyoko Itigi, mkoani Singida, inamilikiwa na kuendeshwa na Wamissionari wa Damu Takatifu ya Yesu, na imekuwa mstari wa mbele katika kuokoa maisha ya watu kwa tiba na kinga ya magonjwa, hasa kwa kutoa kipaumbele kwa ajili ya huduma ya watoto. Hospitali ya Mtakatifu Gaspar, Itigi kwa sasa ina jumla ya vitanda mia nne kwa wagonjwa wanaolazwa, kati ya vitanda hivi, watoto wametengewa vitanda mia tatu.

Akizungumzia kuhusu lengo la mradi huu, Professa David Bocciolini, Rais wa Chama cha Ushirika cha Wakulima wa Legnaia wakishirikiana na Kitivo cha Kilimo cha Chuo Kikuu cha Firenze, Italia, wanataka kuanza kufanya majaribio ya kilimo cha mpunga katika nchi kavu kwa kutumia maji kidogo yanayopatikana katika maeneo ya Sindiga, ambayo hayana uhakika wa mvua na mara kwa mara yanakabiliwa na balaa la njaa.

Pili ni kufanya uchunguzi wa magonjwa yanayoshambulia mazao, ili kuwaongezea tija na mapato wakulima, ili hatimaye waweze kuwa na uhakika wa usalama wa chakula na pato kutokana na shughuli za uzalishaji katika sekta ya kilimo.

Tatu, ni kusaidia kuwaandaa watalaamu watakaoendeleza sekta ya kilimo na ufugaji, ili kuongeza uzalishaji wa maziwa kwa ngo'mbe wanaofugwa kwenye Kijiji cha Matumaini kwa ajili ya matumizi ya watoto walioathirika kwa ugonjwa wa Ukimwi pamoja na wale wanaofugwa Hospitali ya Mtakatifu Gaspar, Itigi. Hii ni kati ya Hospitali za kisasa zilizoko Kanda ya Kati, inayotoa huduma zake hadi vijijini kwa njia ya Zahanati zilizoko chini ya usimamizi wake.

Akizungumza kwenye hafla ya kuchangisha fedha kwa ajili ya Mradi wa Tanzania, Padre Sebastiano Benedettini, C.PP.S, aliwashukuru sana waamini na watu wenye mapenzi mema kutoka Jimbo la Firenze, ambao kwa takribani miaka arobaini, wamekuwa mstari wa mbele katika ujenzi wa utamaduni wa upendo na mshikamano, jambo ambalo limewawezesha Wamissionari wa Damu Takatifu ya Yesu kuanzisha Hospitali na huduma ya maji. Wao ndio waliokuwa wadau wa kwanza wa jitihada hizi za kimissionari chini ya Uongozi thabiti wa Padre Mario Dariozzi, C.PP.S, utamaduni ambao wameuendeleza hadi sasa.

Baadhi ya waamini waliokuwepo kwenye hafla hiyo walisema kwamba, Kwaresima ya mwaka 1976, ilifungua moyo wa ushirikiano na upendo na watu wa Tanzania, katika jitihada zao za kupambana na umaskini, ujinga na maradhi, kwa kuchangia fedha zilizotumika kutengenezea mashine za kusukuma maji, mradi ambao hadi sasa unajulikana kama C.PP.S Mission Water Project, tegemeo la huduma za maji safi na salama kwa wananchi wa mikoa ya Kanda ya Kati Tanzania.







All the contents on this site are copyrighted ©.