2009-01-22 09:39:19

Athari za madawa ya kulevya kwa vijana na jamii


Matumizi haramu ya madawa ya kulevya yana athari zake si tu kwa mtumiaji bali hata kwa familia na jamii kwa ujumla. Padre Flavian Kassala Matindi kutoka Jimbo Katoliki la Geita, Tanzania anapembua kwa kina juu ya madhara ya matumizi haramu ya madawa ya kulevya. RealAudioMP3

Wapendwa vijana,
tunaendela na makala yetu juu ya madawa ya kulevya na madhara yake kwa jamii na kwa namna ya pekee kwa vijana. Baada ya kuwa tumeangalia kwa undani maana halisi ya madawa ya kulevya, hatuna budi leo kuangalia ni nini matokeo ya utumiaji wa madawa haya.

Kwa ujumla hakuna hata faida moja aipatayo mtu kwa kutumia madawa haya. Hali yoyote ya utulivu na kuridhika inayotokea baada ya kutumia madawa haya ni ya mpito tu na kwa kweli ni mwanzo wa safari kuelekea kuharibikia maisha. Mtumiaji yeyote wa madawa ya kulevya hujisikia faraja inayotokana na kusahau mazingira na hasa matatizo yanayomzunguka kwa wakati huo. Hali hii ambayo hudumu kwa muda mfupi tu hufuatiwa na maumivu na hali ya usingizi ambayo humsambabishia mtumiaji mfadhaiko mkubwa wa kimaisha. Ni hali hii ya mfadhaiko inayomsukuma mtumiaji kutafuta tena dozi nyingine ya madawa hayo.

Wataalamu wanaeleza kuwa hali ya utulivu na ugenishwaji wa matatizo binafsi si matunda ya madawa kana kwamba ni kitu kinachosaidia kuachana na matatizo yanayotuzunguka. Kwa kweli kinachotokea ni kwamba madawa ya kulevya baada ya kuwa yametumiwa na mtu yeyote hupunguza uwezo wa kupumua, hushusha mapigo ya moyo na msukumo wa damu. Hali hizi kwa kweli ni safari ya kuelekea katika kuzimia, kuingia katika koma, mapafu kushindwa kufanya kazi yake kwa ufasaha na mwisho wake ni kifo.

Madhara haya yaletwayo na madawa ya kulevya yanatokana na sumu mbalimbali zilizochanganya katika kutengeneza madawa haya. Baadhi ya kemikali zinazotumika katika kuchanganya madawa haya ni pamoja na petroli na maji ya betri za magari na pikipiki yaani sulphuric acid.

Madawa ya kulevya, iwe yale ya kiasili kama bangi au yale yatengenezwayo kimaabala kama vile heroin, husababisha mtu kuwa tegemevu. Mtumiaji wa madawa ya kulevya hufikia mahali ambapo hawezi kufanya jambo lolote bila ya kutumia madawa hayo. Ukizingatia pia bei kubwa ya madawa haya, matokeo ya kwanza kwa mtumiaji ni umaskini. Hali hii ya kuwa tegemevu na umaskini unaotokana na kutumia kila kitu ili kupata madawa haya hufuatiwa na tabia ya wizi, utekaji nyara na tabia zingine zozote haramu ambazo huweza kumpatia mtumiaji vijisenti walau kidogo tu kwa ajili ya kununua madawa ya kulevya.

Pamoja na uharifu, utumiaji wa madawa ya kulevya una uhusiano makubwa sana na maambukizo ya ukimwi. Kwanza kabisa ni kutokana na ukweli kwamba watumiaji wa madawa haya huchangia sindano ambazo wanatumia kwa kujidunga madawa haya. Hali hii husababisha maambukizi ya ukimwi kwa kasi zaida iwapo katika kundi kuna mtu aliyeathirika tayari. Matumizi ya madawa ya kulevya huathiri utashi wa mtu. Na hivyo mtu hutenda mambo yake yote kulingana na hisia zinavyomtuma. Kwa hali hiyo matumizi ya madawa ya kulevya yamekuwa yakihusishwa na matukio mengi ya ubakaji ambao matokeo yake kwa kiasi kikubwa ni kuambukizwa au kuambukiza ukimwi.

Mtume Paulo anatualika kwa upendo na kutukumbusha, “Je hamjui miili yenu ni viungo vya Kristo?” Ni swali linalotupatia changamoto kutafakari kwa kina madhara ya makusudi ambayo yanahatarisha muungano wetu na jamii, na Mungu. Madawa ya kulevya ni sababu kubwa inayochangia mtengano huo hasa kwa vijana katika kizazi chetu hiki. Anandelea kutukumbusha Mtume Paulo “Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu?” Zaidi sana wapendwa vijana mkumbuke kuwa ninyi si mali yenu wenyewe; maana mlinunuliwa kwa thamani. Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu.” (1 Wakor. 6:15 - 20).








All the contents on this site are copyrighted ©.