Sinodi ya Maaskofu iliyokuwa inajadili juu ya Neno la Mungu katika maisha na utume
wa Kanisa, imefungwa rasmi siku ya jumapili kwa Ibada ya Misa takatifu kwenye Kanisa
kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Baada ya kikao, Mababa wa Sinodi wameandika
ujumbe kwa ajili ya watu wa Mungu unaogusa mambo msingi waliyotafakari na hatimaye
kutolea ushauri kuhusu Neno la Mungu kama kiini cha utume wao wakati wote wa Sinodi.
Kimsingi ujumbe huu unawalenga viongozi wa Kanisa waliyopewa dhamana na Mama
Kanisa kuhakikisha kwamba, wanawamegea waamini Neno la Mungu. Ujumbe huu unatumwa
kwa makatekista ambao wamekuwa mstari wa mbele katika kuwasaidia wakatekumeni kulifahamu
Neno la Mungu pamoja na watu wengine wote ambao wamejitoa bila ya kujibakiza kwa ajili
ya kuwasaidia waamini kusikiliza na kulisoma Neno la Mungu. Mababa wa Sinodi wanazama
ndani zaidi katika ujumbe wao, ili kulisaidia Taifa la Mungu, kulipenda na hatimaye,
kujitajirisha na Neno la Mungu. Ili kuifikia azma hii, mambo makuu manne yametiliwa
mkazo na Mababa wa Sinodi katika ujumbe wao kwa taifa la Mungu kwamba: Mosi, Neno
la Mungu ni sauti ya Mungu iliyojidhihirisha tangu mwanzo wakati wa kazi ya uumbaji,
kwa kuvunja kimya na utupu uliokuwepo na hapo Mwenyezi Mungu akaonesha maajabu yake
kwa kuumba ulimwengu. Hii ni sauti ya Mungu inayopenya katika historia ya maisha ya
mwanadamu aliyejeruhiwa kwa uwepo wa dhambi pamoja na kukata tamaa kutokana na taabu
pamoja na kifo. Mwenyezi Mungu anaendelea bado kufanya hija na Taifa lake kwa njia
ya Neema, Agano lake la Milele na kwa njia ya ukombozi. Hii ndiyo sauti inayoingia
katika Maandiko Matakatifu, Inayosomwa Kanisani, kwa kuongozwa na Roho Mtakatifu,
anayetoa mwanga wa ukweli kwa Neno la Mungu na wachungaji wake.
Pili, huyu
ndiye Neno aliyefanyika mwili, kama anavyoandika Mtakatifu Yohane, nasi tumebahatika
kuuona uso wake, Yaani Yesu Kristo, Mwana wa Mungu wa milele. Tumeuona ubinadamu wake,
uliosongwa na mauti, akafungwa katika historia ya nyakati, kati ya watu na nchi inayoweza
kutambulika. Yesu alijitahidi kuuishi ubinadamu wake katika ukamilifu, isipokuwa hakuwa
na dhambi hadi kifo cha Msalaba, lakini akafufuka kutoka katika wafu, kama ilivyoandikwa
na sasa anaishi milele.
Anakamilisha uhusiano kati ya mwamini na Neno la Mungu.
Anamkirimia mwamini uelewa na Umoja unaofumbatwa katika Maandiko Matakatifu, kwa maana
hii, Ukristo ni dini inayopata msingi wa uhai wake kwa Yesu Kristo, anayewafunulia
waamini Mwenyezi Mungu. Anawasaidia waamini kulifahamu Neno la Mungu katika maneno
ya wanadamu, wakijitahidi kujifunza kwa kutumia njia na maneno yao, lakini daima wakitunza
ndani yake ule mwanga wa ukweli wa Kimungu, unaowawezesha waamini kuishi na kutafakari
pamoja na Roho Mtakatifu.
Tatu, Mababa wa Sinodi wanasema, Roho Mtakatifu
anawaongoza waamini katika hija ya maisha yao katika Nyumba ya Neno la Mungu, ambayo
ni Kanisa, kama anavyobainisha Mwinjili Luka, katika kitabu chake cha Matendo ya Mitume
2:42. Ni mahali ambapo waamini wanajichotea Mafundisho ya Neno la Mungu, kwa kusoma
na kujitahidi kuielewa Biblia kwa wote, katika katekesi, mahubiri na utangazaji wa
Neno hili unaogusa akili na moyo wa mwanadamu. Ndani ya nyumba hii, waamini wanashiriki
katika Kuumega Mkate kwa njia ya Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, kama ilivyojidhihirisha
wakati Yesu alipokutana na wanafunzi wa Emmaus.
Waamini wanaalikwa kujitajirisha
kwa Liturjia ya chakula cha Neno la Mungu na Mwili wa Kristo, katika Sakramenti ya
Ekaristi Takatifu. Mababa wa Sinodi wanakumbusha kwamba, hii ni nyumba ya sala inayopambwa
kwa Zaburi, Tenzi na Nyimbo zinazojichotea utajiri wake kutoka katika Neno la Mungu.
Ni nyumba ya Sala ya Kanisa, inayoliwezesha Kanisa kumwimbia Mungu sifa kila siku
na nyakati zote za Mwaka wa Kanisa. Kuna Sala ya Neno la Mungu, inayojulikana kwa
lugha ya Kitaalamu: Lectio Divina, Njia Sala katika usomaji wa Neno la Mungu, kulitafakari
kama njia ya kukutana na Yesu aliye hai. Mwishowe, kuna umoja wa kidugu, kwani kwa
wakristo, haitoshi kusikiliza Neno la Mungu tu, bali wanapaswa pia kulimwilisha katika
maisha yao, kwa njia ya matendo ya mapendo. Kwenye Nyumba ya Neno la Mungu, waamini
wanakutana na ndugu zao kutoka Makanisa na Madhehebu mengine ya Kikristo, hata katika
utengano wao, lakini bado wanaishi katika Umoja wa Kanisa, kwa njia ya kuabudu na
kulipenda Neno la Mungu. Sehemu ya Nne katika Ramani hii ya maisha ya kiroho,
Mababa wa Sinodi wanawakumbusha waamini kwamba, wanatumwa kwenda kutangaza Habari
Njema ya Wokovu hadi miisho yote ya dunia, kwa kuwafundisha kushika yote aliyoamuru
Kristo, yale ambayo wameyasikia katika kificho, wayatangaze juu ya pawa za nyumba.
Neno la Mungu halina budi kuhakikisha kwamba, linaingia hata kwenye njia za mawasiliano
ya Kisasa: Kwenye Familia, ili wazazi na watoto wao waweze kuisoma, kuisali na hatimaye
iwe ni taa katika hija ya maisha yao.
Mababa wa Sinodi wanatoa changamoto
kwamba, umefika wakati sasa Biblia kujipenyeza kwenye shule na taasisi za elimu, kwani
huko ndiko, kwa miaka mingi Neno la Mungu limekuwa ni kiini rejea kwa Sanaa, Machapisho,
Muziki, Fikira na Maadili. Uwezo na utajiri wa Neno la Mungu katika matumizi ya lugha
ya picha, ushairi na simulizi, unakoleza utamu wa imani na utamaduni, katika ulimwengu
ambao kwa kiasi kikubwa unapambwa na ubaya pamoja na upweke. Mababa wa Sinodi
katika ujumbe wao, wanasema, Biblia pia inaonesha taabu zinazoibuka katika uso wa
dunia, hiki ni kilio cha watu wanaodhulumiwa, wanaolalamika kuhusu hali yao ya maisha.
Kilele chake ni pale juu ya Msalaba, Kristo mwenyewe, aliyebaki peke yake baada ya
wafuasi wake wa karibu kutimua mbio, aliweza kuyamimina maisha yake kwa njia ya mateso
na kifo. Lakini kwa vile Yesu ni Mwana wa Mungu, giza la dhambi na mauti linashindwa
kwa Mwanga wa Pasaka, kwa njia ya matumaini na utukufu. Mababa wanawakumbusha waamini
kwamba, katika hija ya maisha yao hapa duniani, ndugu wa kutoka Makanisa mengine pamoja
na madehehbu ya kikristo wanafanya hija hii ya maisha, hata katika hali hii ya utengano,
wanaendelea kuonesha umoja wao kwa kuliabudu na kulipenda Neno la Mungu. Katika hija
hii, wakristo wanakutana na waamini wa dini mbali mbali duniani wanasikiliza kwa makini
na kumwilisha ujumbe wa Vitabu vyao vitukufu, ambao wakiungana pamoja na wakristo,
wanapania kujenga ulimwengu unaosimikwa katika Amani na Mwanga, kwani Mwenyezi Mungu
anapenda watu wote waokoke na kuufahamu ukweli. Mababa wa Sinodi wanawaalika waamini
kulinda Biblia katika nyumba zao, kuisoma, kujifunza kwa dhati kabisa pamoja na kujitahidi
kuuelewa ujumbe wa Neno la Mungu katika maisha, ili uweze kuwasaidia kugeuka na kuwa
ni watu wa sala wanaolitolea ushuhuda, wanaolisikiliza kwa upendo na imani katika
liturjia. Mababa wanawaomba waamini kujenga ukimya, ili Neno la Mungu liweze kupenya
na kufanya makao yake katika maisha ya waamini. Mwangi wa Neno la Mungu usikike katika
maisha ya waamini wanapoianza siku yao na wakati wa jioni, wanapokunja jamvi la maisha
yao ya siku. Mababa wa Sinodi wanahitimisha ujumbe wao kwa Familia ya Mungu kwa
maneno ya Mtakatifu Paulo mtume na Mwalimu wa Mataifa kwa kuwaaga na kusema kwamba:
basi sasa ninawaweka katika mikono ya Mungu, na kwa Neno la neema yake. Mababa wa
Sinodi wanawaaminisha waamini walioenea sehemu mbali mbali za dunia juu ya Neno la
Mungu kama hukumu, lakini zaidi kama Neema, inayoweza kufananishwa na upanga unaokata
kuwili, lakini ni tamu kama sega la asali. Lina nguvu na utukufu, linalowaongoza katika
njia ya Historia pamoja na Yesu, wanaompenda kama wanavyofanya wao.